Katibu Tawala wa Wilaya ya Kigamboni, Bi Pendo Mahalu, ametoa pongezi kwa kundi la wajane kwa namna wanavyojitoa kushiriki katika shughuli mbalimbali za maendeleo ndani ya Halmashauri, akisema kuwa kundi hilo limekuwa mfano wa kuigwa wilayani humo.
Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Wajane Duniani yaliyofanyika kwenye viwanja vya Mji Mwema, Bi Mahalu alisema kuwa Serikali ya Wilaya ya Kigamboni inatambua na kuthamini juhudi za wajane, hasa katika kushiriki kwenye shughuli za kijamii na kiuchumi zinazochochea maendeleo ya wananchi.
“Nawapongeza wajane kwa moyo wa kujitolea. Mmeendelea kuonesha mshikamano na kushiriki kikamilifu katika shughuli mbalimbali kwa manufaa ya jamii yetu. Mmebeba jukumu kubwa la kulea familia zenu na pia kuchangia maendeleo ya wilaya yetu,” alisema Bi Mahalu.
Aidha, alitumia fursa hiyo kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuboresha sera, kanuni na miongozo mbalimbali inayolenga kuweka mazingira rafiki kwa wawekezaji wa ndani na nje ya nchi. Alisema kuwa hatua hizo zimefungua fursa nyingi katika sekta ya viwanda, ikiwa ni pamoja na kutoa ajira kwa wananchi na kuwezesha uuzaji wa malighafi zinazozalishwa Kigamboni.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Wajane wa Wilaya ya Kigamboni, Bi Maimuna Kihiyo ameipongeza Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa kwa namna inavyowawezesha na kuwapa ushirikiano katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili.
“Tunaishukuru sana Halmashauri yetu kwa kutupa nafasi na kutusikiliza tunapohitaji msaada. Ushirikiano huu umetuwezesha kuwa na ujasiri wa kushiriki katika shughuli za maendeleo na kutafuta fursa za kiuchumi,” alisema mwenyekiti huyo.
Naye mdau wa maendeleo wa Wilaya ya Kigamboni, Ndugu Dotto Rweikiza, amewaomba wadau mbalimbali kujitokeza kusaidia makundi maalumu katika wilaya hiyo ili kuwapa motisha na kuwawezesha kiuchumi. Amesema kuwa msaada huo utasaidia kuongeza ushiriki wa makundi hayo katika shughuli za maendeleo na kupunguza utegemezi.
@maendeleoyajamii @gwajima
Gezaulole Kata ya Somangila, Kigamboni
Anuani ya Posta: 36009 Dar es Salaam
Simu: +255222928468
Simu ya Mkononi: +255222928468
Bara pepe: info@kigambonimc.go.tz
Haki Miliki©2017 Manispaa ya Kigamboni . Haki zote Zimehifadhiwa